WAATHIRIKA WA MAFURIKO WA MARA KWA MARA JIJINI ARUSHA WATOA KILIO KINGINE
ARUSHA.
Wakati mvua za masika zikianza kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini;Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Kambi ya Fisi Kata ya Ngarenaro jijini Arusha wanahofia usalama wa maisha yao kufuatia mfereji mkubwa wa mkondo wa
maji ulioelekezwa katika makazi yao.
Wakizungumza na Radio Triple A wakazi hao wamesema kilio
chao ni cha muda mrefu na pia ni changamoto kubwa kwao; hivyo wameiomba
serikali kupitia mamlaka husika kulipatia ufumbuazi suala hilo kwa haraka kabla hawajafikiwa na adha ambazo zimekuwa zikiwakumba kila kinapowadia kipindi cha mvua.
Mwenyekiti wa mtaa wa Kambi ya Fisi Bwana Hillary Mkony
amesema viongozi wakishirikiana na wakazi wa mtaa huo wamekuwa wakijitolea
kuchukua hatua mbalimbali ikiwemo kujenga vivuko lakini kutokana na wingi wa
maji nyakati za mvua bado ni changamoto kubwa kwao.
Kwa upande wake diwani wa kata ya Ngarenaro Isaya Doita
amemuomba Meneja wa TANROADS kwa kushirikiana na wataalamu wake kuharakisha
ujenzi wa mtaro huo kabla ya mvua za masika ili kunusuru maisha ya wananchi
hao.
Meneja wa TANROADS Arusha Mhandisi John Kalupale amekiri
kupokea malalamiko ya wakazi hao na kusema kuwa ni kweli ni kilio cha muda
mrefu na ili kufanikisha ujenzi wa mtaro huo zinahitajika zaidi ya shilingi
milioni mia mbili ambazo tayari wameziomba serikali kuu kwa ajili ya ujenzi
huo.
source.triple a fm habari/27.02.2018


Post a Comment